10/27/2010

Mikutano ya Kampeni Dar es salaam: JK amshitaki aliyemtusi

Na Mgaya Kingoba, Dar es salaam



MGOMBEA Urais wa CCM, Rais Jakaya Kikwete amemshitaki kwa wananchi mgombea ubunge wa Temeke kupitia Chadema aliyemtusi katika mkutano wa kampeni, akiwataka wamnyime kura yeye na chama hicho.

Amewafananisha mgombea huyo na chama chake kuwa majuha waliokata tamaa ndio maana wanatukana, na kuwataka wananchi wajihadhari nao kwa kuwanyima kura.

Rais Kikwete alitoa kauli hiyo kwa nyakati tofauti akihutubia mikutano mikubwa ya kampeni Kiwalani Jimbo la Segerea na Kivule jimboni Ukonga mkoani Dar es Salaam.

“Vinywa vyao vichafu hujapata kuona. Nimeambiwa kwenye mkutano mmoja jana, sijui wapi (baadhi ya wananchi wakajibu Mwembeyanga) kuna mtu alikuwa akivurumisha matusi…mimi nilikuwa safarini.

“Wanazozana tu hao, ni mkusanyiko wa majuha, wameshakata tamaa. Jihadharini nao, dawa yao ni kuwashikisha adabu kwa kuwanyima kura,” alisema Rais Kikwete akihutubia maelfu ya wananchi Kiwalani.

Akiwa katika mkutano wa kampeni jana kwenye Viwanja vya Mwembeyanga, Temeke, mgombea ubunge wa Chadema, Dickson Amos alitumia fursa aliyopewa na mgombea urais, Dk. Willibrod Slaa, kumtusi Rais Kikwete na mama yake.


Akiwa Kivule, alisema siasa ni malumbano ya sera kwa kuwashawishi wananchi namna utakavyoshinda.
 "

Katika mikutano yote hiyo, Rais Kikwete alifafanua Ilani ya Uchaguzi ya CCM kwa mwaka 2010 – 2015 kwa kueleza namna itakavyoshughulikia masuala mbalimbali nchini na katika Mkoa wa Dar es Salaam.

Katika afya, alisema vituo vya afya vya Buguruni na Kivule vitapandishwa hadhi na kuwa Hospitali, na Hospitali ya Wilaya ya Amana itabaki kuwa ya Mkoa.

Alisema zahanati zote za kata zitapandishwa hadhi na kuwa vituo vya afya na vituo vya afya vitapandishwa kuwa hospitali ndogo ili zihudumie watu wengi kutokana na kata za Jiji kuwa na idadi kubwa ya wakazi.

Kuhusu Ukimwi, alisisitiza wananchi wa Dar es Salaam kujihadhari na ugonjwa huo hatari kwa sababu kasi ya maambukizi ni kubwa ikiwa ni asilimia 9.3 na watu 61,443 wanatumia dawa za kupunguza makali ya ugonjwa huo.

Akizungumzia maji, alieleza mikakati ya kuboresha upatikanaji wa huduma hiyo muhimu kwa kuboresha vyanzo vya maji vya Ruvu Juu, Ruvu Chini na Mtoni.

Kuhusu uwezeshaji wananchi kiuchumi, alieleza mikakati ya kuwapatia wafanyabiashara ndogo majengo kama la Machinga lililojengwa Uwanja wa Karume, Ilala, na pia kuendelea kutoa fedha kupitia mifuko mbalimbali.

Alisema katika Mkoa wa Dar es Salaam, vyama vya kuweka na kukopa vimeweza kutoa mikopo ya Sh bilioni 130.

Akiwa Kivule, alikubali ombi la mgombea ubunge wa Ukonga, Eugen Mwaiposa, la kutaka wakazi wa mji huo na ule wa Kipunguni kutohamishwa kwa madai eneo hilo lilitengwa kwa ajili ya kujengwa viwanda.

“Nitawasaidia kulisemea hili katika mamlaka husika. Tutatafuta maeneo mengine ya viwanda, lakini hapa watu wataendelea kukaa, hilo limeishia hapo. Waambieni wawape vibali muishi,” alisema Rais Kikwete na kushangiliwa na maelfu ya wakazi waliohudhuria mkutano huo.

Aliwanadi wagombea wa ubunge wa majimbo hayo, dk. Milton Mahanga na Mwaiposa, na kueleza kuwa wanatosha kushika nafasi hizo, hivyo kuomba wachaguliwe.

Mgombea huyo wa Urais wa CCM atakamilisha kampeni zake Jumamosi, siku moja kabla ya Watanzania kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa nne wa vyama vingi, huku akitabiriwa kupata ushindi.
…siyo kushindana kwa matusi jukwaani, kuchomana visu na kuua. Hawa hawaaminiki kushika madaraka ya nchi, ni sawa na kumpa fisi bucha kulinda,” alieleza Rais Kikwete.
Rais Kikwete alisema katika CCM, hawahubiri kumwaga damu, udini, kutukana wala mifarakano katika jamii kwa sababu mambo hayo hayapo katika sera za chama hicho.

No comments:

Post a Comment