10/17/2010

Mkutano wa Kampeni Manzese: JK aanza kusaka kura Dar



Mgombea urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete akihutubia wakazi wa Manzese Jimbo la Ubungo kwenye mkutano wa kampeni leo mchana.

Mshabiki wa Chama Cha Mapinduzi akionyesha kwa vitendo chaguo lake ni Kikwete kwenye mkutano wa kampeni Manzese mkoani Dar es salaam leo mchana.

Sehemu ya umati wa wananchi waliofurika kuhudhuria mkutano wa kampeni wa Mheshimiwa Kikwete Manzese leo.
 Na Joseph Mwendapole

MGOMBEA urais kwa tiketi ya CCM, Rais Jakaya Kikwete, ameahidi kumaliza msongamano wa magari jijini Dar es Salaam kwa kujenga barabara za juu katika makutano na kuzijenga kwa kiwango cha lami barabara za pembezoni.

Vile vile,amesema serikali inaweka mikakati madhubuti kuhakikisha inatatua tatizo la maji kwa kiasi kikubwa jijini Dar es Salaam kwa kuongeza vyanzo vingi vya uzalishaji maji.

Aliyasema hayo jana katika mikutano yake ya kampeni Manzese na Kawe jijini Dar es Salaam katika mfululizo wa kampeni zake kuelekea Ikulu kwa awamu ya pili.

Alisema barabara za juu zitajengwa katika makutano ya Ubungo, Tazara, Magomeni na makutano ya Chang'ombe lakini vile vile alisema msongamano huo wa magari ni ishara kuwa maisha ya watanzania walio wengi yanaboreka.

Alisema zamani yalikuwa yakionekana magari ya serikali pekee barabarani lakini siku hizi magari mengi yanayoonekana ni ya watu binafsi na kwamba pamoja na kero ya msongamano hiyo ni dalili nzuri kuwa maisha ya watanzania yamepanda.

Aidha, Kikweta alisema barabara kuanzia Moroko hadi Tegeta zitawekwa njia mbili ili kuepusha msongamano ambao hata yeye wakati mwingine unampotezea muda.

"Huwa nikitoka nyumbani Bagamoyo hadi Tegeta pale nachukua nususaa lakini kutoka pale Tegeta hadi Posta inachukua saa nzima kwasababu barabara ni nyembamba sana, zile barabara za pembezoni nazo zitawekwa lami ili watu wasitumie njia moja kwenda mjini," alisema.

Alisema baadhi ya barabara zinazowekwa lami kwa sasa ni pamoja na ile ya Tabata dampo kwenda Kigogo na Ubungo Maziwa kupitia Kigogo na Jangwani kuelekea maeneo ya Kariakoo.

Kuhusu tatizo la maji,Kikwete alisema ndani ya miakamiwili serikali itakuwa imejitahidi kupunguza tatizo hilo kwa kiasi kikubwa kutokana na mipango mikubwa iliyowekwa kwa ajili ya kuongeza vyanzo vya maji.

Alisema mahitaji ya maji jijini Dar esSalaam kwa siku ni lita milioni 50 lakini yanayopatikana kwa sasa ni lita milioni 270 na kwamba jitihada zinachukuliwa kuongeza uzalishaji wa maji Ruvu juu itoke kuzalisha lita milioni 18 kwa siku hadi kufikia lita milioni 60.

Alisema mipango pia inafanywa kuhakikisha mtambo wa Ruvu chini unazalisha lita milioni 90 kwa siku badala ya milioni 40 ambazo zinazaliwashwa kwa sasa.

Alisema serikali inaendelea kutafuta vyanzo vingine vya maji na tayari wameanza kimbiji ambako lita 260 zitakuwa zikizalishwa kwa nguvu za serikali na kushirikiana na serikali ya Norway.

Mgombea huyo alisema serikali pia inafanya mipango kukarabati mifumo ya maji kwani imechakaa na imekuwa ikivujisha maji mengi.

Alisema mifuko ya fedha za mikopo nayo itaendelea kuimarishwa ili wananchi wengi waweze kupata mikopo ya masharti nafuu na kujikwamua kiuchumi kwa kufanya biashara.

Alisema serikali imepanga kujenga 'machinga complex' mbili kila Wilaya zitakazokuwa na uwezo kuchukua wafanyabiashara zaidi ya 40,000 na kwamba kitajengwa kituo kikubwa cha biashara kwenye kiwanja cha Posta ilipo TCRA na tayari bilioni 100 zimeshapatikana kutoka serikali ya watu wa China.

Kuhusu Ukimwi, Kikwete alisema ni mtihani mkubwa jijini Dar esSalaam kwani watu 61,433 wanatumia dawa za kurefusha maisha ARVs na maambukizi katika mkoa huo ni makubwa.

"Ndugu zangu msifanye mzaha na Ukimwi unaua hapa Dar esSalaam maambukizi ni asilimia 9.3 yaani kila watu 100 tisa wana Ukimwi, mzingatie mafundisho ya viongozi wa dini kuacha zinaa na kuwa waaminifu katika ndoa na yaiwashinda kuwasikiliza viongozi wa dini tusikilizeni sisi wahubiri wa dunia tunaowataka mtumie kinga, kinga mkitumia hampati maambukizi na imethibitishwa na wataalamu," alisisitiza Kikwete.

No comments:

Post a Comment