10/26/2010

Mkutano wa Kampeni Nyamagana: Umati mkubwa wafurika kumsikiliza JK


Mgombea Urais wa Tanzania kupitia Chama Cha Mapinduzi Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete akisalimiana na wananchi wa jimbo la Nyamagana alipowasili kwenye mkutano wa kampeni jioni ya leo.



Mapokezi makubwa yamemkaribisha Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete mgombea urais wa Tanzania kwa tiketi ya Chama Cha Mapinduzi jimbo la Nyamagana mkoani Mwanza jioni hii.

Kwenye mkutano wake wa kampeni Mheshimiwa Kikwete alisema CCM ni chama kinachohubiri amani, utulivu na mshikamano na sio chuki na kupigana vita. Hivyo Watanzania wawape nafasi ya kuendelea kuongoza nchi kwa awamu nyingine tena. Alibeza vyama vya siasa vilivyoshindwa kuelezea sera zao na kuhubiri chuki au kutangaza vita.

"Siasa ni ushindani wa sera na mipango ya maendeleo na sio kushindana kurusha mawe na kutupiana matusi kwenye majukwaa" Alisema Mheshimiwa Kikwete huku akishangiliwa na umati mkubwa wa wana Nyamagana waliofurika kwenye uwanja wa Sahara Kata ya Pamba, jimbo la Nyamagana.

Mheshimiwa Kikwete aliyetokea Chato mkoani Kagera, alielezea jitihada za CCM za kuleta maisha bora kwa kila Mtanzania kwa kuboresha huduma za jamii. Alielezea mpango mkubwa wa kusaidia vijiji kumi na mbili vya wilaya hii ya Nyamagana kupata maji safi na salama, unaofadhiliwa na benki ya dunia.

"Miji na Vijiji kumi na nane vitapatiwa umeme katika mkoa huu wa Mwanza ikiwemo Nyamagana na Ukerewe" alieleza Mheshimiwa Kikwete wakati akielezea mpango mkubwa wa kuboresha huduma ya umeme.

Huduma nyingine alizozitolea ufafanuzi ni ile ya ujenzi wa barabara, kilimo kwanza ili kuendeleza wakulima na wafugaji, upanuzi mkubwa wa elimu n.k.

Kabla ya kuhutubia mkutano huo mkubwa wa kampeni, mgombea ubunge wa Jimbo la Nyamagana Mheshimiwa Lawrence Kego Masha aliwahimiza wananchi hao kuwa makini na vyama ambavyo havitawaletea maendeleo na kuwasihi wachague CCM.

No comments:

Post a Comment