9/16/2010

Mkutano wa Kampeni Arusha Mjini: JK aitikisa Arusha!



- Azunguka Uwanja wa Amri Abeid mara mbili akishangiliwa na Maelfu
- Maandamano ya pikipiki na magari yamsindikiza
- Nakaaya Sumari arudi CCM, akabidhiwa kadi na Mwenyekiti


Msafara wa Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete umeingia Arusha Mjini kwa kishindo ambapo maelfu ya wananchi wamefurika kwenye uwanja wa Sheikh Amri Abeid jioni hii.

Baada ya mapokezi hayo ya kishindo, Katibu wa CCM alitangaza kuwa mwanamuziki mashuhurio wa kizazi kipya Nakaaya Sumari ambaye ni mwanachama wa Chadema, ameamua kurudi CCM.

Akiongelea sababu za kurudi CCM, Nakaaya alisema ameamua kwa ridhaa yake mwenyewe kuingia CCM kwa sababu ni chama chenye maendeleo. Alikonga nyoyo za mashabiki wake alipoinmba CCM ina ari zaidi, nguvu zaidi na kasi zaiidi! na kushangiliwa na maelfu ya watu waliofurika uwanjani hapo.

Naye Mwenyekiti wa CCM Taifa na Mgombea urais tiketi ya CCM, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete aliwasihi wananchi wa Arusha kuchagua CCM kwa sababu ni chama cha watu makini.

Akishangiliwa na umati huo, Mheshimiwa Kikwete alikiri kuwa Arusha imefurika kwa umati wa watu na mapokezi makubwa.

Akielezea mafanikio ya CCM kwa miaka mitano iliyopita alisema mafanikio hayo yaliyopatikana kwenye elimu, afya, miundombinu, upatikanaji wa umeme na maji, Mheshimiwa Kikwete alisema zimejitokeza changamoto nyingi na CCM imejipanga kukabiliana nazo kwenye kipindi cha miaka mitano ijayo.

Akizungumzia elimu, alisema CCM imefanikisha ujenzi wa shule za sekondari za kata. Changamoto zilizobaki ni walimu, nyumba za walimu, maabara na vitabu vya kufundishia.

Kwa upande wa vitabu vya kufundishia, Mheshimiwa Kikwete alisema kwa msaada wa Serikali ya Marekani, wamechapisha vitabu vya sayansi vilivyoandikwa na Watanzania vya kutosha wanafunzi wote wa sekondari kwenye masomo ya hisabati, fizikia, kemia na biolojia.

"Hivi ndivyo tutakavyokabiliana na hizi changamoto katika miaka mitano ijayo" alisema.

No comments:

Post a Comment