9/22/2010

Mkutano wa Kampeni Igowole: JK avishwa Mgolole na Viongozi wa Kimila

Mheshimiwa Kikwete akishuka jukwaani baada ya kuhutubia mkutano mkubwa wa kampeni Igowelo leo mchana katika kampeni zake za kutetea kiti chake cha urais kupitia Chama Cha Mapinduzi.
Vikundi vya ngoma wakishangilia ujio wa Mheshimiwa Kikwete Igowelo leo mchana. Pichani chini wana CCM na wananchi wa Igowelo wakimshangilia Mheshimiwa Kikwete alipokuwa akihutubia mkutano wa kampeni.


Mzee Alfonsi Mwinyi Kibuga akielezea wananchi na wageni waliofika Igowole umuhimu wa zawadi za mkuki na kigoda kwa Mheshimiwa Kikwete baada ya kumvika Mgolole - vazi rasmi la wakazi wa eneo hilo.
Baada ya kupokelewa kwa mapokezi ya kishindo, viongozi wa kimila wa Igowole wamemvika mgolole Mgombea Urais kupitia Chama Cha Mapinduzi na Mwenyekiti wa CCM, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete.

Akitambulisha mila hiyo, Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Iringa Bwana Deo Sanga au Jah People Mtu wa Watu, alieleza tenda hilo ni la kihistoria ishara ya watu wa Igowole kumkubali Mheshimiwa Kikwete kama kiongozi wa kitaifa na kumtakia ushindi mnono Oktoba 2010.

Kwa niaba ya wazee wa Igowole, Mzee Alfonsi Mwinyi Kibuga alimvisha mgolole Mheshimiwa Kikwete ambao ni vazi rasmi kwa wananchi wa Mufindi Kusini. Pia alimkabidhi Mheshimiwa Kikwete kigoda kama ishara ya kiti cha uongozi na hatimaye kumpa mkuki kama alama ya ushindi na heshima ya utawala nchi nzima.

Akihutubia umati mkubwa wa wananchi wa Igowole, Mheshimiwa Kikwete aliwashukuru kwa mapokezi makubwa na kwa zawadi hizo za uongozi kutoka kwa wazee hao wa Igowole.

Kama ilivyokuwa kwenye vituo vingine vya mikutano, Mheshimiwa Kikwete alichukua muda mwingi kuasa wananchi kuhusu vita ya kitaifa ya kupambana na UKIMWI ambapo Iringa ni mkoa wenye maambukizi ya juu (wastani wa 15%), mara tatu ya wastani wa maambukizi ya taifa.

Mafanikio yaliyoelezewa ni yale yaliyopatikana kwenye upande wa elimu, afya, upatikanaji maji safi na salama, ujenzi wa barabara na miundombinu mingine. Wakati anafafanua matarajio ya miaka mitano ijayo, Mheshimiwa Kikwete alimuita Mwenyekiti wa CCM Igowole ili aelezee baadhi ya kero za wananchi wa eneo hilo.

Naye mwenyekiti wa CCM Igowole aliomba Barabara ya Igowole mpaka Mtwango ijengwe kwa kiwango cha lami, upatikanaji wa maji safi na mwisho upatikanaji wa ruzuku ya mbolea uongozwe.

Mheshimiwa Kikwete alieleza kuwa ruzuku upatikanaji wa mbolea ya ruzuku umeongezwa kwa asilimia ishirini kwa miaka mitano ijayo. Upande wa maji na barabara aliahidi kulifanyia kazi ili kuhakikisha huduma hizo zinawafikia wananchi.

No comments:

Post a Comment